Mtu mmoja amepoteza maisha baada ya kupigwa na watu wasiojulikana kisha miguuni kwake kufungwa mbuzi aliye hai katika eneo la Nsalala Kata ya Mbalizi Mkoani Mbeya.


Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya Nyagesa Wankyo alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kumtaja marehemu kuwa ni Robart Mwasenga (35) ambaye aliuawa juzi usiku baada ya kupigwa na mtu au watu wasiojulikana kwa tuhuma za wizi.

Inadaiwa kwamba Marehemu huyo kabla ya kufikwa na mauti alifika kwenye banda la mifugo linalomilikiwa na Wilson Mwangasani ambaye ni jirani yake na kutaka kuiba mbuzi.


Afisa Mtendaji wa Kitongoji cha Nsalala Lwitiko Mwaibindi, amesema alipata taarifa kutoka kwa raia mwema, kwamba kuna mtu anahitaji msaada wa haraka kwani anaonekana amepigwa na kuumizwa.

Amesema badaa ya kuona hali hiyo alilazimika kukimbia hadi kituo cha polisi kwa lengo la kutoa taaraifa hizo majira ya saa 5 usiku ambapo hata hivyo alikuta kituo kimefungwa kwa muda huo.

Amesema baada ya kutumia jitihada binafsi kwa kugonga mlango hatimaye alifunguliwa na mmoja wa askari baada ya dakika 15 tangu afike kituoni hapo na kupokewa kwa kauli za vitisho kutoka kwa askari huyo ambaye hakuwa tayari kumtaja jina akidai kuwa mwenyekiti huyo amekiuka taratibu kwani muda wa kazi huishia saa 4 usiku hivyo alipaswa kufika asubuhi.

Aidha baada ya askari kumtaka mwenyekiti kurudi kesho yake hali ilibadilika ambapo kulitokea majibizano yaliyopelekea mwenyekiti kuwekwa mahabusu hadi saa 8 mchana siku iliyofuata.

Amesema kitendo cha yeye kuwekwa mahabusu pamoja na askari kushindwa kufika eneo la tukio kwa muda huo kumechangia kwa kiasi kikubwa marehemu kupoteza maisha kwani kulikuwa na uwezekano wa kupona endapo angewahishwa hospitali.

Hata hivyo baada ya sakata hilo kati ya polisi na mwenyekiti, hatimaye mtendaji wa kitongoji alilazimika kufika kituo cha polisi na kumuwekea dhamana mwenyekiti wake majira ya saa 8 chana .

Akijibu tuhuma hizo,Kaimu kamanda wa polisi Mkoa wa mbeya Nyigesa Wankyo amekiri kupokea taarifa hizo na kuahidi kuzifanyia kazi lakini mwili wa marehemu umeshafanyiwa uchunguzi na kukabidhiwa kwa ndugu zake tayari kwa maziko.

Shiriki nasi kwa kutoa maoni yako hapa chini

Facebook Blogger Plugin by Michapo Blog

Post a Comment

 
Top